Na
Eleuteri Mangi-MAELEZO
Mtoto
huanza kujifunza kulingana na mazingira yake yanayomzunguka, mafunzo hayo
yanamuwezesha kupata uzoefu wenye athari ya kujenga akili, tabia ama uwezo wa
kimaumbile ili aweze kuyamudu mazingira yake.
Hali
hiyo inajenga dhana ya kupata elimu kulingana na mazingira ambayo hujulikana
kama elimu isiyo rasmi.
Ni
vema ikaeleweka kwamba tunapozungumza kuhusu watoto, tunazikusudia jinsia zote
mbili, yaani watoto wa kike na wale wa kiume. Katika hali halisi ndani ya
maisha ya kijamii, elimu ni nyenzo ambayo hutumiwa kupitisha maarifa, ujuzi na
maadili kutoka kwa kizazi kimoja hadi kingine bila kujali jinsia.
Elimu
kwa watoto wa kike ni moja ya njia bora za kupunguza umaskini katika mataifa
yanayoendelea ikiwemo Tanzania.
Manufaa
hayo ya elimu kwa watoto wa kike yanaweza kuonekana kwa mtu binafsi, familia
zao, jamii yote na taifa kwa ujumla.
Ni
dhahiri, manufaa yanayopatikana kupita elimu ni mengi katika jamii ikiwemo
kupunguza idadi ya watoto ambao wanawake hujifungua, kupunguza idadi ya vifo
vya watoto wadogo, kupunguza idadi ya vifo vya akina mama, kuwalinda dhidi ya
maambukizo ya VVU/UKIMWI na kuongeza idadi ya wanawake wenye kazi na mapato ya
juu ambayo hudumu kwa vizazi vingi.
Hakika
ukimuelimisha mtoto wa kike, umemsaidia kuwa na uwezo wa kufanya maamuzi bora
kwa manufaa yake, familia yake na hata taifa.
Hali
hii imechukua sura mpya nchini Tanzania ambapo Serikali, watu binafsi,
mashirika ya dini na taasisi mbalimbali za ndani na nje ya nchi
zimekuwa mstari wa mbele kuhakikisha mtoto wa kike anapata elimu ambayo ndiyo
kinga na urithi pekee ambao hawezi kunyang’anywa wala kugawana na mtu mwingine
ndani ya familia na hata jamii inayomzunguka.
Sura
hiyo mpya imeoneshwa na Mfuko wa Graca Machel (Graca Machel Trust) ambao
umejikita katika kusaidia wanawake na watoto nchi kadhaa Barani Afrika.




