Wizara yangu
inaendelea kutoa taarifa ya wiki kwa umma kuhusu mwenendo wa ugonjwa wa
kipindupindu hapa nchini. Hadi kufikia tarehe 24 Januari 2016, jumla ya watu 14,608 wameugua ugonjwa huo, na kati yao watu 228 wamepoteza maisha kwa ugonjwa huu. Njombe, Ruvuma na Mtwara ndiyo Mikoa
pekee ambayo haijawahi kuripoti mgonjwa yoyote wa kipindupindu, tangu mlipuko
huu uanze mnamo mwezi Agosti mwaka huu.
Kwa mujibu wa Takwimu
za kuanzia tarehe 18 hadi 24 Januari 2016, ni kuwa jumla ya Mikoa ambayo
imeripoti kuwa na wagonjwa ni 15 ambapo
idadi ya wagonjwa 524 na vifo 10 vimeripotiwa. Idadi ya wagonjwa
walioripotiwa wiki hii imepungua ukiliinganisha na idadi ya wiki iliyoishia
tarehe 17 ambapo kulikuwa na wagonjwa 621
na vifo 14 ambalo ni punguzo la
asilimia (16%). Mkoa wa Morogoro bado umeendelea kuripoti idadi kubwa zaidi
ya wagonjwa ukilinganishwa na Mikoa mingine, (Manispaa ya Morogoro 89,
Halmashauri ya Morogoro 36, Mvomero 17), ukifuatiwa na mikoa ya Mwanza (Ukerewe 36, Nyamagana 19 na
Ilemela 13), Simiyu (Bariadi DC 29
na Bariadi municipal 23), Manyara
(Simanjiro 48), Mara (Musoma Manispaa
11, Musoma DC 8, Rorya 8 na Butiama 8), Geita
(Geita DC 21 na Geita TC 6) na Mbeya (Kyela 26).
Mikoa mingine ambayo
bado pia imeendelea kuripoti wagonjwa ni pamoja na Dodoma
(Wagonjwa 22), Arusha (21), Tabora (18), Singida (18), Lindi (12), Rukwa (7),
Kilimanjaro (6) na Kagera (2).