Thursday, January 07, 2016

WAZIRI WA NCHI OFISI YA RAIS TAMISEMI MHE. GEORGE SIMBACHAWENE (MB) AMEMUAGIZA MKURUGENZI WA MANISPAA YA ILALA KUMSIMAMISHA KAZI KAIMU AFISA BIASHARA WA MANISPAA YA ILALA BW. DENNIS. N. MREMA


Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI Mhe. George Simbachawene (Mb) amemuagiza Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala kumsimamisha kazi mara moja Kaimu Afisa Biashara wa Manispaa ya Ilala Bw. Dennis. N. Mrema kuanzia leo tarehe 07 Januari, 2016 kwa kosa la kusababisha upotevu wa Mapato ya Serikali kutokana na urasimu wa kukusudia, mazingira ya rushwa na uzembe katika utoaji wa leseni za Biashara.

Kutokana na hali hiyo Mhe. Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI ameelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala kumuondoa kwenye nafasi yake Kaimu Afisa Biashara wa Manispaa ya Ilala na nafasi yake kukaimiwa na mtu mwingine ili kupisha uchunguzi zaidi juu ya tuhuma zilizotolewa dhidi yake.

Mhe. Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais –TAMISEMI amefikia uamuzi huu baada ya kupokea malalamiko mengi kutoka kwa Wafanyabiashara ambao wamemlalamikia Mtendaji huyu kwa ukiukwaji wa Sheria, Kanuni na Taratibu za utoaji wa Leseni za Biashara, Urasimu na Mazingira ya rushwa.